Naibu Waziri wa Mawasiliano Sayansi na Teknolojia, January Makamba amesema angependa kuona nafasi ya wasanii ikiwa ni pamoja na kulindwa ka haki zao, inatajwa kwenye Katiba Mpya.
Makamba alisema ni vyema kama wasanii watatajwa na kutambuliwa katika Katiba Mpya kama moja ya makundi maalumu, huku kikiwekwa kipengele maalumu cha kulinda na kuendeleza haki za Miliki Bunifu.
“Kama mnavyojua, sasa tunaandika Katiba Mpya, ni nafasi ya kipekee ya kutengeneza taifa jipya. Kwenye rasimu yametajwa makundi mbalimbali, lakini hakuna wasanii. Sanaa ni biashara kubwa ambayo ripoti ya WIPO ya mwaka 2012 inaonyesha kuwa mchango wa mapato uliotokana na shughuli za hakimiliki yalikuwa zaidi ya mchango wa sekta ya madini, umeme, gesi, maji, usafirishaji, mawasiliano, ujenzi, afya na ustawi wa jamii,” alisema Makamba.
Alisema wasanii ndiyo wamekuwa wakilipa jina na utambulisho taifa la Tanzania.
“Maisha ya taifa na urithi wa taifa inahifadhiwa katika kazi za sanaa, iwe ni katika nyimbo, mashairi, michoro, riwaya au maigizo na kazi nyinginezo. Taifa lisilotambua na kuthamini kazi za sanaa ni kwamba halijitambui,” alisema January Makamba.
0 comments:
Post a Comment