Leo katika historia Jumapili, 17 Jamadul-Awwal, 1436 Hijria

Leo ni Jumapili tarehe 17 Jamadul-Awwal mwaka 1436 Hijria, sawa na tarehe 8 Machi 2015 Miladia.
Siku kama ya leo miaka 47 iliyopita, inayosadifiana na 8 Machi 1968 ilianza Harakati ya Ukombozi ya Moro dhidi ya utawala wa dikteta Ferdinand Marcos nchini Ufilipino. Dikteta Marcos alikuwa mshirika na muitifaki mkubwa wa Marekani na katika utawala wake wa kidikteta, maelfu ya Waislamu wa Ufilipino waliuawa au kufungwa jela. Harakati ya Ukombozi ya Moro ilipambana kwa ajili ya kupigania haki za Waislamu, na ilihesabiwa kuwa harakati kubwa zaidi iliyopinga utawala wa Marcos nchini Ufilipino. Baada ya Marcos kuondoka madarakani mwaka 1986, harakati ya Moro ilikubali kutia saini makubaliano ya amani na serikali ya Manila.

Siku kama ya leo miaka 1145 iliyopita, yaani mwaka 291 Hijiria, alifariki dunia Abul-Abbas Ahmad bin Yahya, mtaalamu maarufu wa lugha na nahau. Abul-Abbas katika masomo yake alibobea katika ulingo wa fasihi ya Kiarabu na baada ya miaka kadhaa ya kufanya utafiti wa kina, akatokea kuwa mtaalamu mkubwa katika uwanja huo. Miongoni mwa athari zilizobakia kutoka kwa mtaalamu huyo, ni pamoja na kitabu maarufu kiitwacho ‘I’raabul-Qur’an’.
Siku kama ya leo miaka 986 iliyopita, alizaliwa Muhammad Ghazali msomi wa fiq'hi na mwanafalsafa mashuhuri wa Kiislamu wa Iran. Ghazali alisoma elimu ya fiq'hi kwa Abu Nasri Ismail na alikuwa mmoja wa wasomi wakubwa wa Kiislamu katika elimu hiyo akiwa na umri wa miaka 28. Umaarufu wa Imam Muhammad Ghazali ulipelekea kiongozi wa Iraq wakati huo Khawaja Nidham al-Mulk kumualika msomi huyo kwenda mjini Baghdad kwa ajili ya kufundisha. Hatimaye alirejea Iran na kujishughulisha na masuala ya ualimu. Imam Muhammad Ghazali aliandika kitabu chake maarufu cha "Ihyau Ulumud-Din," mwaka mmoja kabla ya kurejea Iran. Vitabu vingine mashuhuri vya msoni huyo ni "Kemia ya Saada" na "Nasaha za Wafalme."
Na siku kama ya leo miaka 178 iliyopita, alizaliwa Sayyid Muhammad Ali Shah Abdul-Adhim, maarufu kwa jina la ‘Hidaayat Husseini’, faqihi na alimu mkubwa wa Kiislamu. Hidayat Husseini alisafiri mjini Najaf, Iraq ambapo kwa miaka kadhaa alipata kusoma kwa Sheikh Murtadha Answari, aliyekuwa mmoja wa mafuqahaa wakubwa katika ulimwengu wa Kiislamu. Hidayat Husseini, alibobea katika elimu ya Hadithi na wapokezi wa hadithi, huku akiandika vitabu vingi mojawapo kikiwa ni ‘Wasilatur-Ridhwaan’. Msomi huyo alifariki dunia mnamo mwaka 1343 Hijiria huko mjini Najaf.
Share on Google Plus

About nellychazzy

I Run And Own Nellychazy.blogspot.com. Working With Web Editing, Blogs Template Fix And Editing (HTML). Monitoring click4hosting.net Deals with Web hosting. Also Base On Software And Hardware, Phones,Computer
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Blogger Tricks