Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi NACTE limefuta usajili wa vyuo 13 na kuvishusha hadhi vyuo 60 ambavyo vimekiuka sheria ya usajili.
Vyuo vingine vimebainika kutoa mitaala isiyosajiliwa na vyuo hivyo na vingine kutokuwa na sifa za kuendesha mafunzo ya ufundi.
Baraza hilo lenye mamlaka ya kusimamia elimu ya ufundi nchini limesema bado linavifanyia uchunguzi vyuo vingi nchini ili kuona kama vina tija ya kuendelea kutoa elimu inayokidhi mahitaji ya soko la ajira kimataifa.
Katibu Mtendaji wa Baraza hilo Dokta Primus Nkwera amebainisha hayo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa jengo jipya la mitihani lililojengwa na Baraza hilo kwa kushirikiana na Serikali kwa gharama ya shilingi bilioni 2.7.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dkt Shukuru Kawambwa ndiye aliyezindua jengo hilo na amesema kuwa Sera mpya iliyobuniwa na Wizara yake itasaidia kuondokana na udanganyifu kwenye baadhi ya vyuo nchini.
Kwa upande wake Kaimu Mwenyekiti wa Baraza hilo Mhandisi Steven Mlote amesema Baraza limefungua ofisi kwenye kanda saba nchini ili kuweka huduma jirani na maeneo ya vyuo pamoja na kukagua na kuhakiki viwango vya ubora wa vyuo vya elimu nchini.
0 comments:
Post a Comment